MISS TZ NA.3 AFUNGUKIA USHINDI WA SITTI

Gumzo mtaani kwa sasa kwenye ulimwengu wa urembo ni ushindi wa mwanadada Sitti Abbas Mtevu ambaye hivi karibuni aliibuka mshindi katika Shindano la Miss Tanzania 2014. Tutakumbuka baada ya Sitti kutangazwa mshindi, maneno yalikuwa mengi, mara alipendelewa, mara alidanganya umri, wengine wakasema eti ana mtoto.
Miss Tanzania namba tatu, Jihan Dimachk.
Yameongelewa mengi na kimsingi mpaka sasa bado ushindi wake unaonekana kuwa na makengeza. Kutokana na hali hiyo, waandishi wetu walifanya mazungumzo na baadhi ya wadau lakini kati yao alikuwa mmoja wa washiriki ambaye alichukua nafasi ya tatu, huyu ni Jihan Dimachk.
Kwenye fainali za mashindano hayo mrembo huyu alichukua Taji la Miss Tanzania Top Model 2014 na sasa fuatilia exclusive enterview hii iliyofanyika kati yake na Ijumaa ndani ya Hoteli ya Regency iliyopo Mikocheni, Dar.
Ijumaa: Habari yako Jihan, sisi ni waandishi kutoka Gazeti la Ijumaa.
Jihan: Okey, nashukuru kuwafahamu, karibuni.
Ijumaa: Tuanze na matokeo ya kinyang’anyiro cha Miss Tanzania mwaka huu, unadhani wewe ulistahili kuchukua nafasi ya tatu na Sitti Mtemvu kuibuka kidedea?
Jihan: Siwezi kuongea sana jamani lakini kwa kifupi nilikuwa nikiamini nitashinda, niseme tu kwamba it was unfair but I can’t explain (haikuwa sawa ila siwezi kuelezea).
Ijumaa: Kwa nini unasema hivyo? hebu fafanua kauli yako.
Jihan: Sipendi kuwa muongeaji sana, naheshimu maamuzi ya majaji na Kamati ya Miss Tanzania lakini ukweli uliopo moyoni mwangu ni kwamba nilijiamini na ndiyo maana niliingia kwenye kinyang’anyiro nikijua ushindi ni haki yangu.
Ijumaa: Wapo wanaosema ulikuwa na kila kigezo cha kuwa Miss Tanzania 2014 lakini umetoswa kutokana na rangi yako ukihisiwa wewe si Mtanzania, unaliongeleaje hili?
Jihan: Sipendi kabisa kusikia maneno hayo, mimi ni Mtanzania, nimezaliwa Mwanza, mama yangu ni Msukuma na baba yangu Mlebanon. Tangu naingia kwenye shindano hili waandaaji walinihoji, wakafuatilia hilo na kutambua ni Mtanzania, ingekuwa tofauti sidhani kama ningeruhusiwa kushiriki.
 Ijumaa: Kwa mfano ikitokea Sitti akavuliwa taji kutokana na haya yanayozungumzwa, uko tayari uvishwe wewe?
Jihan: Siwezi kulijibu swali hilo kwani haijatokea. Endapo itatokea na waandaaji wakanifuata kuniambia hivyo, hapo ndiyo nitakuwa na la kuzungumza.
Ijumaa: Unamuongeleaje Sitti Mtemvu?
Jihan: Kwa sababu ndiye aliyevishwa taji, naheshimu ushindi wake, namkubali kuwa ni mrembo na siwezi kupingana na maamuzi yaliyotolewa.
Ijumaa: Umechukua nafasi ya tatu ambayo nayo si haba, una mipango gani ya baadaye?
Jihan: Nina mambo mengi ya kufanya. Nina ndoto za kuwasaidia wanawake na watoto lakini pia nahisi nina jukumu la kusaidia katika suala la elimu nchini, nitajipanga kufanikisha hayo.
Ijumaa: Kwa nini elimu?
Jihan: Nimekuwa nikikutana na watu wengi ambao elimu imekuwa kikwazo kwenye maisha yao, nikawa nimejiapiza kuhakikisha nawasaidia kadiri nitakavyoweza.
Ijumaa: Asante sana Jihan, tunakutakia mafanikio katika yale unayopanga kuyafanya.
 Jihan: Nashukuru sana

CHANZO; GPL
Share on Google Plus

About EDITOR

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment